WAZIRI Mkuu, Mizengo Pinda, Akiri kwamba Serikali ilifanya uzembe katika kutatua taarifa za uchochezi zilizosababisha vurugu za Mtwara.., Soma Zaidi



WAZIRI Mkuu, Mizengo Pinda, amekiri kwamba Serikali ilifanya uzembe katika kutatua taarifa za uchochezi zilizosababisha vurugu za Mtwara. Kauli hiyo aliitoa mjini Mtwara  jana alipozungumza na wananchi wa Masasi akiwa njiani kuelekea wilayani Nanyumbu kufungua mradi wa umeme. Alisema baada ya kutokea kwa uzembe huo wako wajanja wachache waliotumia nafasi hiyo kufanikisha malengo yao.

“Katika hili tulizidiwa ujanja na watu wengine kwa kuwa walikuwa wakiwaambia wananchi kwamba gesi itatolewa Mtwara na kupelekwa Dar es Salaam.

“Tena wakasema ikishafikishwa Dar es Salaam ambako vitajengwa vinu na gesi nyingine itapelekwa Bagamoyo kwao Rais Jakaya Kikwete.

“Huo ulikuwa ni upotoshaji mkubwa tena mkubwa kweli lakini sisi tulilichukulia juu juu, hatukutazama kwa undani kulieleza hilo na wajanja wakalipata na kulipotosha hilo,” alisema Pinda.

Alisema gesi itazalishwa Mtwara ingawa vinu vitajengwa Dar es Salaam kwa ajili ya kuisambaza gesi hiyo kwa watumiaji wengine.

“Wakati nazungumza na watu wa Mtwara mwaka jana, walinieleza mambo mengi sana juu ya hiyo gesi na mwishowe nikawauliza hivi kwanini hamtaki gesi itoke Mtwara.

“Nikawauliza, hivi ikija meli hapa Mtwara ikapaki pale bandarini na kupakia gesi na kuipeleka Uarabuni mtakataa, wakasema hatuna shida, nikawauliza tena je, meli hiyo hiyo ikipakia gesi na kuipeleka Dar es Salaam, mna tatizo, wakasema hatuna tatizo.

“Sasa nikawauliza tatizo lenu ni nini, wakasema ni hilo bomba lenu hilo mnalojenga. Mimi nikawaambia gesi itazalishwa hapa Mtwara, tena katika Kijiji cha Madimba na itakayopelekwa Dar es Salaam haitazidi asilimia 10.

“Nikawambia gesi ikianza kuzalishwa mtanufaika kwa kuwa hata viwanda vitakuwapo kikiwamo cha Dangote kitakachozalisha saruji pale Kijiji cha Msijute,” alisema Pinda.

Kuhusu hasara iliyopatikana baada ya wananchi kufanya vurugu na kuharibu mali, alisema bado inafanyiwa kazi na itakapokamilika italetwa mkoani Mtwara.

“Baada ya vurugu zile, Serikali ilifanya tathimini ya matukio na ikiwezekana kabla ya mwisho wa mwaka wa fedha huu itakuwa imekamilika na tutaangalia la kufanya ingawa nataka niwahakikishie kwamba jambo hili tunalifanyia kazi na litakapokamilika tutalirudisha kwenu,” alisema Pinda.

Aliwashukuru viongozi wa Mkoa wa Mtwara kwa kutochukua uamuzi wa kulipa kisasi wakati wa vurugu hizo kwa kuwa kama wangeamua kufanya hivyo hali ingekuwa mbaya zaidi.

Awali, Mkuu wa Wilaya ya Masasi, Farida Mgomi, alisema vurugu hizo zilizotokea Januari 26, 2013 zilisababisha hasara ya Sh bil 3.4.

>>Mtanzania

0 comments: