WANANCHI WENYE HASIRA KALI WATIA KIBERITI NYUMBA ZA MBARALI ESTATES HUKO MBEYA..

Nyumba tano kuchomwa moto, wizi wa mali na watu kupigwa, ni sehemu ya matukio yaliyotokea katika vurugu za kutisha katika Mji wa Ubaruku wilayani hapa, Mbeya, juzi jioni.

Vurugu hizo zimekuja  baada ya wakazi wa eneo hilo kukasirishwa na kifo cha mtoto wa umri miaka 14 anayedaiwa kupigwa na walinzi wa mwekezaji wa Kampuni ya Mbarali  Estates.

 Nyumba zilizochomwa ni  za mlinzi mkuu  wa kampuni,  Atanas Pelela, mgambo wa kituo kilichomo ndani ya kampuni, Ramadhani Mwamuli na ya  Ofisa Uhusiano wa kampuni, Ignasi Mgao.

Pia nyumba ya  Edison Joseph  ambaye hana uhusiano na kampuni, lakini hivi karibuni alihama kisiasa kutoka Chadema na kujiunga na CCM,jambo ambalo alisema anahisi kuwa ni kiini.

Nyumba ya mtu aliyetambuliwa kuwa ni Mafikiri Mwanishuri ilipigwa mawe na kupasuliwa vioo vya madirisha na yeye mwenyewe kujeruhiwa na sasa amelazwa katika Hospitali ya Ikonda, wilayani Makete.

 Hata hivyo polisi wamefanikiwa kudhibiti vurugu hizo na watu 50 wanashikiliwa.

Tukio hilo lilitokea juzi saa 12:00 jioni na habari za awali zilisema  vurugu  hizo ziliwalenga zaidi walinzi wanaodaiwa kumpiga na hatimaye kusababisha kifo cha mtoto Lusajo Anosisye (14).

 Mtoto huyo anadaiwa kupigwa na kujeruhiwa sehemu mbalimbali na inasemekana kitendo hicho kilifanyika Oktoba wakati akikatisha kwenye eneo la kampuni hiyo.

Kwa mujibu wa habari hizo baada ya kupigwa mtoto huyo alilazwa katika Hospitali ya Wilaya ya Mbarali hadi alipofariki dunia juzi jioni. Maziko yalitarajiwa kufanyika jana.

Diwani wa Kata ya Ubaruku, George Mbillah, alithibitisha tukio hilo huku akibainisha kwamba mtoto alipigwa Oktoba 29 mwaka huu

 Mbillah alisema taarifa za awali zilisema mtoto huyo alipigwa baada ya kupita kwenye  njia inayokatisha eneo la shamba wakati akipita kwenda kukata matete porini .

Inadaiwa baada ya kipigo hicho, mtoto huyo alichukuliwa na mkurugenzi wa shamba hilo na kumpeleka kituo cha polisi na kudaiwa  mwizi .Kwa mujibu wa habari hizo, polisi walimpeleka mahabusu  katika  Gereza la Rujewa.

Diwani huyo alisema mtoto huyo aliwekewa dhamana,lakini alipotoka aliendelea kuumwa na baadaye kupelekwa katika Hospitali ya Rujewa ambako alifariki juzi.

Baada ya habari kuhusu kifo cha mtoto huyo, wananchi walitaharuki  na kuamua  kuchoma moto nyumba.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mbeya, Diwan Athuman, alisema watu 50 wamekamatwa wakihusishwa na tukio hilo.

-Mwananchi